بسم الله الرحمن الرحيم


بسم الله الرحمن الرحيم

UDOMSA.

Wednesday 15 September 2010

SUALA LA MUSTABATION

Suali:
Nini athari na hukumu ya kufanya kitendo cha masturbation ktk uislam,au je inaruhusiwa?
Naomba unifahamishe.

Jawabu:
Maulamaa wanasema kuwa Kitendo cha Masturbation (kuitowa manii kwa njia ya mkono) ni haramu kwa mwanamke na mwanamume, na dalili ni kauli ya Mwenyezi Mungu (Subhanahu wa Ta'ala) Aliposema:
 ( وَالَّذِينَ هُمْ لِفُرُوجِهِمْ حَافِظُونَ . إِلا عَلَى أَزْوَاجِهِمْ أوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُهُمْ فَإِنَّهُمْ غَيْرُ مَلُومِينَ ) المؤمنون/5، 6
Na ambao wanazilinda tupu zao (kwa kutofanya kitendo cha jinsia), Isipo kuwa kwa wake zao au kwa iliyo wamiliki mikono yao ya kulia. Kwani hao si wenye kulaumiwa
Al Muuminun – 5-6

Anasema Imam Ash-Shafi'iy (Mwenyezi Mungu Amrehemu):
"Kitendo cha masturbation ni haramu kwa sababu ni kitendo cha jinsia, kwa ushahidi wa aya hii, na haijuzu kutenda kitendo cha jinsia isipokuwa kwa hao waliotajwa katika aya hiyo. Na MwenyeziMungu akakamilisha kwa kusema: "Lakini anaye taka kinyume cha haya, basi hao ndio warukao mipaka, Al Muuminuun – 7
Ikafahamika kuwa haijuzu kutenda kitendo cha jinsia isipokuwa kwa mke au kwa waliomiliki mikono ya kulia, na kwa hivyo haijuzu kuitowa manii kwa njia ya mkono – WaLlahu A'alam."
Kitaab Al-Umm – Imam Shafi

Katika kuwaepusha watu na kitendo hiki Mwenyezi Mungu Ametuambia:
وَلْيَسْتَعْفِفِ الَّذِينَ لا يَجِدُونَ نِكَاحًا حَتَّى يُغْنِيَهُمْ اللَّه
Na wajizuilie na machafu wale wasio pata cha kuolea, mpaka Mwenyezi Mungu Awatajirishe kwa fadhila yake.
Annur – 33

Aya hii inawataka wasio na uwezo wa kuowa wajitahidi katika kujizuwia na machafu (kikiwemo kitendo hicho cha masturbation) mpaka pale Mwenyezi Mungu Atakapowafungulia milango ya fadhila Zake.

Kutoka kwa Ibni Mas'uud (Radhiya Llahu anhu) anasema:
"Tulikuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) na sisi wakati huo tulikuwa vijana tusiokuwa na utajiri, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) akatuambia:
"Enyi vijana! Kila mwenye uwezo wa kuowa kati yenu basi aowe, kwa sababu kunamuepusha na kutizama (ya haramu) na kunalinda tupu zake, na kwa asiye na  uwezo wa kuowa, basi afunge kwa sababu kufunga kunaondoa hamu ya kufanya kitendo cha jinsia."
Al-Bukhaariy na wengine

Ili kujiepusha na kufanya kitendo hiki ni vizuri mtu kufuata yafuatayo:
·        Kwanza kabisa kumbuka kuwa mtu hawezi kukifanya mbele ya sahibu zake wala ahli yake wala hata watu asiowaheshimu. Anakifanya akiwa amejificha mtu yeyote asimuone kwa sababu anajuwa fika kuwa hicho ni kitendo cha aibu. Lakini mtu huyo anasahau kuwa Mwenyezi Mungu Anamuona.
Mwenyezi Mungu Anasema:
( يَسْتَخْفُونَ مِنَ النَّاسِ ولا يَسْتَخْفُونَ مِنَ اللَّهِ وَهُوَ مَعَهُمْ) النساء/ 108
Wanataka kujificha kwa watu, wala hawataki kujificha kwa Mwenyezi Mungu, Naye Yu pamoja nao
·        Kumdhukuru Mwenyezi Mungu rohoni na mdomoni mara kwa mara.
·        Mume arudi kwa mke haraka sana au amchukuwe mkewe na aishi naye ni bora kuliko kuwa mbali muda mrefu kukasababisha ghadhabu ya Mwenyezi Mungu juu yao.
·        Kujishughulisha na mambo yenye manufaa na nafsi yake na wanadamu wenzake na akhera yake.
·        Kujiepusha kutizama yaliyoharamishwa kama vile picha, filam na mengine yenye kuzidisha hamu ya kutaka kufanya kitendo hicho.
·        Kuutumia wakati usiokuwa na kazi kwa kusoma Qurani au kuswali au kusoma vitabu vyenye faida.
·        Kuiondowa ile fikra ambayo vijana wengi wanayo kuwa; eti masturbation inaruhusiwa ikiwa itakuepusha kufanya kitendo cha zina nk.
·        Kuongeza nguvu ya nafsi yako 'will power' na kujiepusha kubaki peke yako wakati mwingi kama alivyotufundisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).
·        Kufuata mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) kwa kufunga.
·        Kulala mapema
·        Kuwa mvumilivu kwa kutegemea malipo mema kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
·        Zidishe kufanya Istighfaar kila wakati na penda kuitamka kauli hii:
لا إلهَ إِلاَّ اللَّهُ وَحْدَهُ لا شَرِيكَ لَهُ، لَهُ المُلْكُ وَلَهُ الحَمْدُ وَهُوَ على كُلّ شَيْءٍ قَدِيرٌ
Ndani ya kauli hii mna kheri nyingi sana.

No comments:

Post a Comment